Friday, 23 March 2018

Halmashauri ya Wilaya Ya Hai yatoa mikopo ya fedha kwa vikundi kumi na moja



 
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai Bi Helga Mchomvu

HAI

Jumla ya vikundi  11 vya kina mama na  vijana wilayani Hai mkoani Kilimanjaro vimepokea hundi ya mikopo ya jumla ya shilingi milioni 30 kutoka kwenye asilimia kumi ya mapato ya halmashauri kama inavyoelekezwa na serikali.

Akikabidhi hundi hizo kwa vikundi hivyo mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Hai Bi. Helga Mchomvu amewataka wanufaika wa mikopo hiyo kuzitumia pesa hizo ipasavyo kwa miradi ya uzalishaji ili waeweze kurejesha fedha hizo ili wakina mama wengine na vijana waweze kunufaika.

Amesema kuwa baadhi ya vikundi vinashindwa kufikia malengo ya kukua kiuchumi kutokana na baadhi yao kuelekeza fedha hizo katika matumizi binafsi yasiyokuwa ya uzalishaji ikiwa ni pamoja na baadhi yao kufanyia anasa jambo ambalo linakwamisha mpango wa utoaji huo kufikia malengo yake.

Mchomvu ameongeza kuwa madiwani wanaotoka katika kata za vikundi  vilivyopokea  mikopo hiyo kuhakikisha wanafuatilia kwa ukaribu mienendo ya miradi hiyo na kuhakikisha matumizi sahihi yanafanywa kama ilivyokusudiwa.

Kwa upande wake Husna Thomas  ambaye ni mwenyekiti wa kikundi cha Amani kilichopo kijiji cha Chekimaji  kata ya Masama Rundugai wanaojishughulisha na uuzaji wa mpunga na maharage ameishukuru serikali kwa kutenga asilimia hizo kwa wanawake na vijana jambo ambalo litawasaidia kutatua changamoto za kiuchumi.

Naye Mohamed Yusuph ambaye ni mwenyekiti wa kikundi cha mbalamwezi katika kata ya Bomang’ombe ameahidi kusimamia fedha hizo katika kikundi ili ziweze kutumika ipasavyo kwenye miradi mbalimbali ya kimaendeleo na kujikwamua kiuchumi.

Awamu inayo kuja Baraza la Madiwani la halmashauri hiyo limekusudia kutenga asilimia mbili toka katika asilimia kumi na kuzielekeza kwa watu wa makundi maalumu hasa walemavu ili nao waweze kunufaika na mikopo hiyo kutatua changamoto zinazo wakabili.

No comments:

Watumiaji wa Barabara Watakiwa Kutii Sheria za Usalama

Mkuu wa Kitengo cha Usalama barabarani Mkoa wa Kilimanjaro Mrakibu Msaidizi wa Polisi Sauda Mohamed akizungumza na wananchi kwenye ...