Na Omary Mlekwa
HAI
HAI
HALMASHAURI ya wilaya ya Hai, Mkoani Kilimanjaro, imetumia zaidi ya shilingi bil 13 ambayo ni sawa na asilimia 34 ya makisio ya bajeti ya mwaka 2017/2018 ya mapato na matumizi ya shilingi bil 38.
Akitoa taarifa ya mapato na matumizi ya mwaka 2017/2018 kwa kamati ya ushauri ya wilaya hiyo,kaimu ofisa Mipango, Erick Marishamu,alisema matumizi hayo ni hadi kufikia desemba 31 mwaka 2017.
Alisema matumizi yatokanayo na mapato ya ndani ni shilingi milioni 487 sawa na asilimia 18 ya makisio ya shilingi bilioni 2.7 huku matumizi ya utekelezaji wa miradi ya Maendeleo ni shilingi milioni 555 sawa na asilimia 10 ya makisio ya shilingi bilioni 5.9.
Alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto ya utekelezaji wa bajeti hiyo kutokana na kuchelewa kupokelewa kwa fedha za ruzuku ya uendeshaji na ruzuku ya miradi ya Maendeleo pamoja kutopokelewa kabisa kwa fedha zilizoidhinishwa katika bajeti.
"Mheshimiwa Mwenyekiti uelewa mdogo wa wafanyabiashara katika ulipaji wa kodi na ushuru kwa wakati pamoja na baadhi ya vyanzo kuondolewa na kuelekezwa vikusanywe na mamlaka ya mapato nchini (TRA) vyanzo vilivyoondolewa ni pamoja na kodi ya majengo ,ushuru wa mabango" alisema.
Aidha ,alifafanua kuwa mikakati ya utatuzi wa changamoto hizo hizo katika bajeti hiyo ni kuendelea kukusanya kwa kutumia oparesheni maalamu ya kushtukiza pamoja na kuunda timu za ukusanyaji wa mapato katika ngazi mbali mbali za vijiji ,kata na Halmashauri.
No comments:
Post a Comment